EPL yaweka wazi tarehe ya kuanza mazoezi, angalia mikakati itakayozingatiwa ili wachezaji wasiambukizane corona

285

Wakati Ligi Kuu England ikikusudia kurejea rasmi Juni 8 na mazoezi kuanza katikati ya mwezi Mei kuna mambo ambayo viongozi wa ligi hiyo wamekusudia vilabu kutekeleza kabla ya mashindano rasmi kuanza.

Corona ipo na bado haijulikani itakoma lini hivyo viongozi wa EPL wanataka EPL ichezwe bila mashabiki lakini ichezwe na bingwa apatikana kiuhalali.

Pale England wameweka haya mambo yatakayozingatiwa kwenye mazoezi na baada ya mazoezi:-

Mosi, wachezaji watapimwa mara mbili kwa wiki huku watatazamwa dalili za COVID-19 kila siku.

Vipimo vyote vitachukuliwa na wabobezi wa afya kutoka hospitali ya taifa NHS ambao watasambaza vifaa katika kila uwanja wa vilabu hivyo.

Mazoezi yatafanyika bila wachezaji kukaribiana sawa na njia nyingine za kujikinga zitafuatwa vyema kabisa.

Wachezaji wanatakiwa waingie mazoezi wakiwa wamevalia nguo za mazoezi tayari huku wakiwa wamevalia barakoa kila muda.

Hawatakiwi kuoga klabuni au kula pamoja. Kama klabu inahitaji kuwapa wachezaji chakula basi kiwe cha kupewa kwenda kula nyumbani au sehemu nyingine (takeaway).

Huduma muhimu pekee itaruhusiwa kwa wachezaji itaruhusiwa, ambapo NHS watakuja wakiwa wamevalia PPE.

Licha ya mikakati hiyo tayari Ligi Kuu Ufaransa ilishafutwa huku PSG akipewa ubingwa, Uholanzi Ligi pia imefutwa bila kuwepo kwa bingwa kutokana na timu hizo kufungana kwa alama pale juu kwenye msimamo, na Ligi ya Ubeligiji pia imefutwa.

Author: Bruce Amani