Man United Yakubali, Yaishe Casemiro Atatumikia Kadi Nyekundu na kukosa mechi nne
Manchester United wameweka wazi kuwa hawatakata rufaa kupinga maamuzi ya refarii wa mchezo wa Ligi Kuu England dhidi ya Southampton ambao ulimalizika kwa sare tasa huku Casemiro akionyeshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja.
Refarii Anthony Taylor alionyesha kadi ya njano lakini baada ya mapitio ya VAR akabadilisha maamuzi na kutoa kadi nyekundu ambayo inamfanya mchezaji huyo wa zamani wa Real Madrid ya Hispania kukosa mechi nne mfululizo.
Awali kulikuwa na taarifa kuwa, United watapinga uamuzi huo lakini kwa taarifa ambazo zimetolewa jioni ya leo zinaeleza Manchester United kutokuwa na nia ya kuendelea kupinga maamuzi ya waamuzi.
Inakuwa ni mara ya pili kwa Casemiro kuonyeshwa kadi nyekundu kwenye kikosi cha Manchester United ambapo ameifikia rekodi ya Nemanja Vidic kuonyeshwa kadi nyekundu zaidi ya mara moja kwa msimu mmoja.
Casemiro atakosa mchezo dhidi ya Fulham Kombe la FA, atakosa mechi dhidi ya Newcastle United, Brentford na Everton za EPL.
