Mwanariadha Pistorius kuomba aachiliwe mapema kutoka jela
Mwanariadha wa zamani wa Afrika Kusini aliyekuwa bingwa katika michezo ya Olimpiki ya walemavu Oscar Pistorius aliyefungwa jela mwaka 2016 kwa kumuua mpenzi wake Reeva Steenkamp, ataiomba bodi ya msamaha leo imuachie huru mapema kutoka jela. Haya yamesemwa na mawakili wake na maafisa wa gereza.
Msemaji mmoja wa magereza amethibitisha kwamba kunaendelea kikao cha faragha cha bodi ya msamaha katika gereza hilo. Kulingana na wakili wa familia ya Steenkamp, familia hiyo inapinga ombi hilo la msamaha na itatoa taarifa katika kikao cha kusikilizwa kwa ombi hilo kueleza jinsi mauaji hayo yalivyoiathiri familia hiyo.
Pistorius alipewa kifungo cha miaka 13 jela na ana haki ya kuruhusiwa kuondoka gerezani baada ya kutumikia nusu ya kifungo hicho.
