FC Talanta Yamsajili Kuta, Dola Kutoka Mathare United

Siku moja baada ya kutangazwa kuwa mchezaji huru na Mathare United kiungo Augustine Kuta amepata makaazi mapya ambayo ni FC Talanta na atakuwepo hapo katika kipindi ambacho hakijawekwa wazi.

Kuta ni mmoja tu ya wachezaji ambao wametua FC Talanta katika dirisha hili ingawa kwake kuondoka Mathare United ni kutafuta nafasi zaidi ya kucheza baada ya kuonekana akiwa klabuni hapo kuwa kama fungu la kukosa.

Mathare United mwishoni mwa wiki iliyopita walitangaza kuachana na wachezaji sita kati ya wachezaji hao alikuwepo Kuta wengine walikuwa ni Samson Otieno, Mustapha Oduor, Valdo Madegwa, Reagan Onyango, na Dennis Isukwe.

Kuta amejiunga na FC Talanta ambayo imekuwa na uchumi mgumu huku ikipoteza idadi kadhaa ya wachezaji wake muhimu akiwemo Vincent Otieno na Dennis Oalo, ikielezwa kuwa wachezaji hawajalipwa karibia mwaka sasa.

Wachezaji wengine ambao wametua klabuni hapo ni mlinzi wa Sofapaka Samuel ‘Dola’ Olwande na aliyekuwa nahodha wa Vihiga Bullets Lucas Waitere.

Author: Asifiwe Mbembela