Tusker FC Wazitaka Alama Tatu za Wazito FC

Kocha Mkuu wa Tusker FC Robert Matano amepanga kuvuna alama nyingine tatu mbele ya Wazito FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya KPL utakaochezwa Jumatano katika uwanja wa Ruaraka majira ya saa tisa.

Tusker wanahitaji alama hizo ili kuendelea kuipatia presha Gor Mahia ambao ni vinara wa Ligi Kuu nchini Kenya kwa hivi sasa.

Endapo watashinda kwenye mechi hiyo, mabingwa watetezi Tusker wataenda kileleni mwa msimamo wa KPL kwa kufikisha pointi 54 na kuwa alama moja zaidi ya vinara wa sasa Gor Mahia.

Katika takribani miezi miwili iliyopita, Tusker wamekuwa na mwendelezo wa ushindi ambapo wameshinda mechi sita mfululizo, tano zikiwa mechi za ligi, moja kwenye Kombe la Mozzart Bet hatua ya 16 bora dhidi ya Rainbow.

“Mchezo wetu ujao tutacheza na Wazito, ni timu ngumu lakini nadhani tutampango wa kukabiliana nao na kukusanya alama kwa namna yoyote ile”, alisema Matano kocha mwenye wasifu mzuri nchini Kenya kwa hivi sasa.

Author: Asifiwe Mbembela