Gor Mahia kugharamia pakubwa utundu wa mashabiki wake

Kamati huru ya kinidhamu na malalamishi ya KPL (IDCC) imeipiga timu ya Gor Mahia faini ya shilingi za Kenya 906,000 kutokana utovu wa nidhamu wa mashabiki wa timu hiyo katika mechi mbili za ligi kuu nchini Kenya – KPL

Mnamo tarehe 27 Januari mjini Machakos, mashabiki walisababisha kusitishwa kwa mechi yao na timu ya KCB kwa muda waliporusha mawe uwanjani katika dakika za mwisho za mechi. Mashabiki hao pia waliharibu ukuta wa ndani kwenye uwanja huo, na vile vile kusababisha uharibifu wa magari mawili ya wagonjwa. Aidha basi la timu ya KCB ilivunjwa kioo cha nyuma.

Gor sasa watagharamia uharibu huo. IDCC imewaamuru kulipa laki tatu kwa utovu wa nidhamu, shilingi elfu hamsini na Sita kugharamia marekebisho ya ambulensi, shilingi elfu hamsini kugharamia ukuta ulioharibiwa na shilingi elfu mia mbili itakayotumiwa kuirekebisha basi la KCB.

Katika Kesi ya pili, Gor italipa shilingi laki tatu kutokana na mashabiki wao kuingia uwanjani wakati wa mechi kati yao na maasimu wao wa jadi AFC Leopards mwezi Agosti mwaka uliopita. Kulingana na IDCC, Gor Mahia ulishindwa kuwadhibiti mashabiki wao na uvamizi huo wa ugani uliyaweka maisha ya wachezaji na waamuzi wa mechi kwenye hatari

Author: Kevin Teya