Bocco wa Simba kinara upachikaji mabao VPL

377

Nahodha wa klabu ya Simba John Raphael Bocco amewapongeza wachezaji wenzake ndani ya klabu hiyo kwa ushirikiano aliopata hasa kutoka kwa washambuliaji Medie Kagere na Chris Mugalu.

 

Bocco amesema ulikuwa msimu bora kwao kama washambuliaji pamoja na wachezaji wote na kila aliyepata nafasi alifunga na ni moja ya chachu iliyosababisha ubingwa wa msimu huu.

 

Nahodha huyo ameongeza kuwa ushirikiano baina ya wachezaji, benchi la ufundi, viongozi na mashabiki umechangia mafanikio ya msimu huu.

 

“Kwa dhati niwapongeze washambuliaji wenzangu Kagere na Mugalu kwa ushirikiano walionipa hadi leo, ilikuwa aliye kwenye nafasi anapewa pasi na anafunga.

 

“Tulikuwa na msimu mzuri, ushirikiano ulikuwa mkubwa kuanzia wachezaji viongozi hadi mashabiki na hilo limechangia pakubwa kufanikisha hili,” amesema Bocco.

 

Bocco amemaliza akiwa kinara wa ufungaji kwa kutupia kambani mabao 16 akifuatiwa na Mugalu mwenye 15 huku Kagere akifunga 13.

 

Kuwa kinara kwa Bocco kunahitimisha kiatu cha dhahabu ambacho kilienda kwa Kagere msimu uliopita.

Author: Asifiwe Mbembela